MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Ally Samatta jana ametokea benchi KRC Genk ikiibuka na ushindi wa 3-0 dhidi ya Kortrijk kwenye mchezo wa Kundi B kuwania tiketi ya kucheza michuano ya UEFA Europa League mwakani.

Samatta aliingia dakika ya 66 kwenda kuchukua nafasi ya mfungaji wa bao la kwanza la Genk jana, kinda Mbelgiji, LeandroTrossard aliyefunga kwa penalti dakika ya 14 katika mchezo huo ambao mabao mengine yalifungwa na kinda mwingine Mbelgiji, Siebe Schrijvers mawili, dakika ya 45 na 70.

Samatta alianzia benchi jana baada ya mchezo uliopita kuanzishwa Jumatano, lakini hakufunga KRC Genk wakilazimishwa sare ya 1-1 na wenyeji, AS Eupen Uwanja wa Kehrweg mjini.

Genk inaendelea kuongoza Kundi B katika mchuano wa kuwania tiketi ya Europa League kwa pointi zake 16 sasa baada ya kucheza mechi sita na Samatta jana ameiichezea Genk mechi ya 55 tangu ajiunge nayo Januari mwaka jana kutoka TP Mazembe ya DRC akiwa amefunga mabao 18.

Kati ya mechi hizo 55, michezo 18 Samatta alicheza msimu uliopita na 37 msimu huu na kati ya hiyo, ni michezo 33 tu ndiyo alianza, 10 msimu uliopita na 23 msimu huu.

Mechi 21 kati ya hizo alitokea benchi, nane msimu uliopita na 13 msimu huu, wakati 11 hakumaliza baada ya kutolewa, tano msimu uliopita na sita msimu huu na katika mabao hayo 18, 12 amefunga msimu huu na sita msimu uliopita.

Kikosi cha Genkkilikuwa; Ryan, Nastic, Colley, Dewaest, Castagne, Berge/Malinovskyi dk73, Heynen, Writers, Trossard/Samatta dk66, Buffalo na Naranjo/Boëtius dk81.

KV Kortrijk : Kaminski, Goutas, De Smet/Ivanof dk65, Chevalier, Van Der Bruggen, Rougeaux, Rolland, Ouali, Totovytskyi D'Haene na Sarr/Stojanovic dk45.

Tupia Comments: