Mkuu  wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai wa Wilaya (OCCID), Yustino Mgonja ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwa alimkamata Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu baada ya Mkuu wa Upelelezi Kanda Maalumu (ZCO), Camilius Wambura kumtaka afanye hivyo.

Mgonja ambaye ni shahidi wa nne katika kesi ya kutumia lugha ya uchochezi inayomkabili Lissu, alidai hayo jana mbele ya Hakimu Mkazi, Godfrey Mwambapa kesi hiyo ilipokuja kwa ajili ya kusikilizwa.

Akiongozwa na Wakili Mwandamizi wa Serikali, Mutalemwa Kishenyi, shahidi huyo alidai kuwa Juni 28, mwaka jana, Wambura alimpa maelekezo ya kumkamata Lissu kwa kosa la kutoa lugha za uchochezi katika viwanja vya mahakama hiyo.

Alidai kuwa Juni 29 mwaka jana saa 7 mchana alienda nyumbani kwa Lissu maeneo ya Tegeta wilayani Kinondoni, ambapo alimkamata na kumfikisha katika ofisi ya ZCO na kumkabidhi.

“Nilipewa amri na ZCO nikukamate hivyo kwa mamlaka hayo bila kuwa na hati ya ukamataji naweza kukukamata; kwani makosa yoyote ya jinai unaruhusiwa kukamata bila kuwa na hati hiyo,” alidai Mhonja.

Pia alidai kuwa kumpinga Rais anapokosea sio kosa na kwamba tafsiri ya maneno aliyoyatoa, ndio yamesababisha kukamatwa na kushitakiwa kwa kutumia lugha za kichochezi.

Katika mashitaka yake, Lissu anadaiwa kuwa Juni 28, mwaka huu akiwa katika viwanja vya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, alitoa kauli za uchochezi kuwa “Mamlaka ya Serikali mbovu ni ya kidikteta uchwara inahitaji kupingwa na kila Mtanzania kwa nguvu zote, ‘huyu diktekta uchwara lazima apingwe kila sehemu’. Kama uongozi utafanywa na utawala wa kijinga nchi inaingia ndani ya giza nene.’’

Tupia Comments: