SIKU zote katika uhusiano matendo yetu ndio yanayoweza kututabiria namna uhusiano mzima utakavyokuwa ama wa kudumu au ndio utaishia njia panda na kuacha majeraha. Kadri unavyojiingiza katika uhusiano ni lazima ujipange na kuhakikisha kwanza lengo lako la kuwa kwenye uhusiano husika.
Wengi hujikuta wakiwa katika majonzi, majuto na kukata tamaa ya mapenzi kutokana na ukweli kuwa walishindwa kujipanga na kudhibiti matendo yao mbele ya wenza wao wakati wakiwa kwenye uhusiano.
Jambo la msingi, pale unapoamua kuingia kwenye uhusiano baada ya kujipanga ni muhimu kuchukua tahadhari kadhaa kuhakikisha unafanya mambo ambayo hayataibua migongano na baadaye kupelekea uhusiano husika kuvunjika.
Kwanza kabisa, ni muhimu kuondokana na matarajio makubwa dhidi ya mwenza wako. Wengi wanapoingia kwenye uhusiano huwa na matarajio makubwa ya uhusiano husika kwa maana ya ndoa hali inayosababisha kuwa ving’ang’anizi na wakati mwingine kufikia kuwa hadi kero.
Si vibaya unapokuwa kwenye uhusiano tena wa muda mrefu ukaona hakuna dalili ya uhusiano huo kuwa kudumu, kuanza kuchukua tahadhari lakini jambo la msingi ni kufuata utaratibu mzuri ambao hautoleta usumbufu kwa mwenza wako. Lakini matarajio mengine ni ya kifedha au mali dhidi ya wenza wetu.
Wapo watu wanaojiingiza kwenye uhusiano wakiwa na matarajio Mahusiano na ndoa nyingi huyumbishwa na matarajio yasiyo halisi kabla hata ya kuingia katika mahusiano na hatimaye ndoa wengi wetu huwa na matarajio binafsi ya kimaisha.
Matarajio haya yanajumuisha vile tunavyotaka sie wenyewe kuwa hapo baadaye, pamoja na matarajio ya vile tunavyotaka wenza wetu wawe. Kutokana na hali hiyo, wengi wetu hujikuta wakiwa na matarajio ya kuwabadili wenza wao ili wawe na hali fulani wanayoitaka wao, na kusahau kuwa hata hao wenza wetu nao wana matarajio yao.
Matokeo yake katika uhusiano husika kunatokea tatizo la ukinzani wa matarajio kutokana na kuwepo kwa mgongano na mwisho wa siku inaibuka vita. Hivyo basi, ili kuwa na uhusiano wa kudumu ni vyema kupeana nafasi wenza ya kila mtu kutimiza ndoto zake, na ikiwezekana saidianeni kufanikisha ndoto zenu kwa kuwa mwisho wa siku mafanikio ya kila mmoja wenu ni mafanikio ya uhusiano huo.

Tupia Comments: