WATANZANIA 1,009 ambao walikuwa nguvukazi ya taifa wamefungwa vifungo vya maisha katika magereza mbalimbali nje ya nchi.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ametoa takwimu hizo jana wakati akifunga Maadhimisho ya Kitaifa ya Siku ya Kupiga Vita Dawa za Kulevya Duniani katika Viwanja vya Nyerere Square mkoani Dodoma. Alisema serikali haitagharamia kuwarudisha nchini wafungwa hao ambao wengi wao ni vijana, lakini kwa taifa linalotaka ujenzi wa uchumi wa viwanda, limepoteza nguvukazi muhimu katika kujenga uchumi wake.

Waziri Mkuu ambaye ni Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la Kudhibiti Dawa za Kulevya, alisema nchi 21 ambako Watanzania hao wamefungwa ni China watu 265, ambapo kati yao 68 wamehukumiwa kunyongwa. “Nyingine ni Afrika Kusini watu (296), Brazili (121, Kenya (660, Irani (630, India (260), Uturuki (38), Ugiriki (250, Uingereza na Ireland (24) Msumbiji (20), Malasia na Tailand (16), Pakistani (15), Uganda (15), Japan (6), Nepal (4), Comoro (3), Misri (2) na Indonesia, Hispania, Ghana, Nigeria amefungwa mmoja mmoja kila nchi,” alisema.

Alisema tangu Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya ilipoanza Februari mwaka huu hadi mwezi huu, imefanya jitihada kubwa na mabadiliko dhidi ya dawa ya kulevya yameonekana, ambapo ekari 565.75 za mashamba ya bangi katika mikoa mbalimbali nchini zimeteketezwa. “Mikoa inayoongoza ni pamoja na Mara (Tarime na Rolya) ekari 156.75, Morogoro (78), Arusha (68), Kagera (57) na Ruvuma ekari 35.

Aidha, kilo 11,307 za mirungi zimekamatwa na ekari 64.5 za mashamba ya mirungi zimeteketezwa katika mikoa ya Kilimanjaro, Kagera na Mbeya,” alisema. Waziri Mkuu alisema katika kipindi hicho, kilo 1,815 za heroini na kilo 27.58 za kokeni zimekamatwa na katika kipindi hicho hadi kufika Mei mwaka huu, lita 12,890 za kemikali bashirifu zinazotengeneza heroini na kokeni zimekamatwa.

Alisema mamlaka hiyo pia imebaini mbinu mbalimbali za magendo za dawa za kulevya, ikiwemo matumizi ya kemikali bashirifu kwa ajili ya kuzibadilisha na kutengeneza dawa za kulevya. Alisema taifa halitamwacha salama mtu yeyote anayejishughulisha kuanzia wazalishaji, wasambazaji, wauzaji na hata watumiaji wa dawa za kulevya na kifungo chake ni miaka 30.

Tupia Comments: