Rais wa China Xi Jinping amemwapisha kiongozi mpya wa Hong Kong, Carrie Lam, katika sherehe za kuadhimisha miaka 20 tangu Uingereza ilivyoukabidhi mji huo kwa utawala wa China.
Bendera za China na Hong Kong zilipeperushwa katika sherehe hizo zilizofanyika nje Jumamosi, ambapo ziliadhimishwa mbele ya bandari ile ile, mahali ambapo gavana wa mwisho wa Uingereza alikabidhi madaraka kwa uongozi wa China mwaka 1997.
Mtendaji mkuu mpya wa Hong Kong aliyepitishwa na Beijing, Lam aliapa Jumamosi kuitumikia China na Hong Kong. Kiongozi huyo alichaguliwa kwa kura chini ya asilimia moja ya wapiga kura wa Hong Kong, katika mchakato ambao wanaharakati wa demokrasia wameupigia kelele kuwa kimsingi haukuwa wa haki.
Mamia ya polisi walipangwa kulinda sherehe hizo, siku ambayo kwa kawaida watu huandamana Hong Kong. Mapambano yalitokea kati ya wanaharakati wanaofagilia demokrasia na wale ambao wanafungamana na serikali ya Beijing, katika maandamano yaliyofanyika kilomita kama moja kutoka kwenye sherehe za kuapishwa kiongozi huyo mpya.
Hali ya ulinzi imeimarishwa sana kwa ajili ya ziara ya Xi ya siku tatu katika mji huo. Xi amesema atakutana na watu wa kila namna wakati wa ziara yake, lakini kutokana na ulinzi kuwa mkali inaelekea kuwa waandamanaji wengi na sauti zao za kutaka mageuzi inawezekana zisisikike wala wao kuonekana.
Uingereza ilirejesha mji wa Hong Kong kwa utawala wa China Julai 1, 1997, chini ya utaratibu wa nchi moja, mifumo miwili ambayo ina hakikisha uhuru mpana kwa ajili ya mji huo ambao hawapati raia wa bara nchini China.
Ijumaa, waziri wa mambo ya nje amesema hati iliyokuwa imesainiwa na Uingereza na China ambayo ilianzisha makabidhiano hayo haitumiki tena.”

Tupia Comments: