Wakati Afrika ikikabiliwa na hali mbaya ya ukame, na tishio la njaa likiwaelemea mamilioni ya watu, wataalamu wanakutana kwenye Jukwaa la Uchumi Duniani (WEF) kuzungumzia suala la usalama wa chakula Afrika.
Wakiwa mjini Durban Afrika Kusini wataalamu hao wamesema kuwa suala la usalama wa chakula ni lazima liwe ni sehemu kubwa ya mazungumzo katika kulisukuma mbele bara la Afrika kiuchumi.
Mwandishi wa VOA anaripoti kuwa ziko tayari juhudi mahsusi zinazofanyika katika kuhamasisha aina mpya ya wakulima wa kiafrika, wanaojulikana kama Wakulima wafanya biashara. (agripreneurs).
Mkutano wa WEF unaofanyika kila mwaka Switzerland kwa kawaida ni tukio lenye kuhudhuriwa na viongozi wakubwa, lakini katika mkutano wa jumuiya ya kimataifa wiki hii, wahusika wakuu wa bara la Afrika wanawakaribisha wakulima wadogo ambao sasa wanajulikana kama “agripreneur”

Mchumi wa kilimo Paul Makube, ambaye anafanya kazi na First National Bank ya Afrika Kusini, ameiambia VOA inaleta tija kuzungumzia kilimo wakati panapo zungumziwa kujenga masoko yenye ushindani, na kuboresha ubunifu na teknolojia.

“Ili biashara iweze kustawi, inahitaji hali ambayo ya utulivu, na kuhusu usambazaji wa chakula na pia uzalishaji, kwa kanda mbali mbali za Kusini mwa Afrika na Afrika kwa ujumla,” amesema Makube.

Wachumi na wataalamu wa kilimo wanasema, janga la chakula linalo ikabili Afrika hivi sasa haliwezi kubebesha lawama juu ya ukame peke yake ambao umeathiri sehemu kubwa ya bara hilo.

Ukame pamoja na vita kubwa zimewaangamiza mamilioni ya watu ambao wanakabiliwa na janga la njaa nchini Somalia, Sudan Kusini na Ziwa Chad huko Afrika Magharibi.
Lakini, wataalamu wanasema, kuna tatizo kubwa katika ukulima wa Kiafrika—hasa, wanasema wataalamu, kushindwa kwa wakulima wa chakula kujihusisha katika biashara zenye kuwapa faida.

Vikwazo hivyo ni pamoja na kukosekana miundo mbinu ya kufikisha bidhaa hizo katika masoko, ushindani unaoletwa na vyakula vinavyo ingizwa kutoka nje, sera za serikali ambazo hazitoi msaada wa kutosha kwa wakulima, kutokuwepo kwa bima ya wakulima, na kushindwa kwao kupata teknolojia.

Shirika la Grow Africa partnership linafanya juhudi kuongeza uwekezaji binafsi katika sekta ya kilimo, na mkurugenzi wake mtendaji, William Asiko, amesema ameona mafanikio ya kilimo cha ushirika katika nchi yake ya Kenya.

“Kuwasaidia wakulima wadogo wadogo wa kilimo cha kibiashara kuna faida kubwa zaidi kwa nchi mbalimbali, bila shaka tayari imeonyesha mafanikio katika Afrika Mashariki, ambapo kuna wakulima wa chakula na hivi sasa wanazalisha cha ziada kwa juhudi zote zilizofanyika na kuwaletea ufanisi,” amesema Asiko.

Ni katika kuhakikisha kuwa mifumo ya vyama vya ushirika vinafanya kazi vizuri ili kwamba wakulima waweze kupata mavuno mazuri, kupata bei nzuri katika soko na pia waweze kufanya kazi na wasindikaji wa vyakula na kuhakikisha kuwa sera hizo zinafanya kazi kwa ajili ya kuwawezesha kuwekeza na kufanya kazi pamoja na wakulima hawa.”
Na tatizo ni makundi maalum ya watu, anasema Birju Patel wa kampuni ya Export Trading Group yenye makazi yake Afrika Kusini.

“Kwa wastani umri wa wakulima wadogo wadogo Afrika ni kati ya miaka 60-65. Na huo ni umri wa mtu kusataafu kwa kila mmoja wetu aliyekuwa katika chumba hiki, sawa? Sasa, vipi utaweza kuwashawishi vijana kujihusisha na kilimo? Kwa hivyo hiyo ndio changamoto kubwa kwetu hivi sasa,” amesema Patel.

Ameongeza kuwa bila shaka tukitaka kusonga mbele kama ambavyo watu wengine duniani wanavyopiga hatua, tunahisi teknolojia ndio itakuwa na mchango mkubwa katika hilo.”
Kuongeza idadi ya agripreneurs wa mazao siku za usoni halitakuwa jambo jepesi, wanasema wataalamu. Itataka kuwepo kwa wawekezaji wakubwa katika fedha, muda, na ufuatilaiji, lakini wanasema tija ya juhudi hii ni muhimu katika kulisha bara ambalo uchumi wake unakua.

Tupia Comments: