Ripoti zinasema kuwa takriban watu 140 ikiwemo raia huenda wamefariki katika shambulio katika kambi moja ya wanahewa nchini Libya.
Ilikuwa imedaiwa kuwa huenda watu 60 walifariki wakati wapiganaji wanaounga mkono serikali walipojaribu kuiteka kambi ya Brak al-Shati siku ya Alhamisi.
Waziri wa ulinzi wa serikali inayoungwa mkono na Umoja wa Mataifa na kamanda wa jeshi wote wamesimamishwa kazi wakisubiri uchunguzi.
Waziri mkuu amekana kuagiza shambulio hilo.
Msemaji wa jeshi alisema kuwa wameiteka kambi hiyo na kuharibu vifaa vyote vilivyokuwa ndani.
Meya wa mji huo alisema kuwa ndege zilizokuwa ndani ya kambi hiyo zilichomwa.
Wengi waliofariki walikuwa wanajeshi wa kundi la Libyan National Army LNA, muungano wa eneo la mashariki la taifa hilo ambao hautambui serikali katika mji mkuu wa Tripoli.
Wapiganaji hao walikuwa wakidhibti kambi hiyo tangu mwezi Disemba.
Msemaji wake alitoa idadi ya waliouawa kuwa 140.
Wanajeshi hao walikuwa wakirudi kutoka katika gwaride la kijeshi. hawakuwa na silaha.
''Wengi wao waliuawa'' ,alisema.
Mjumbe wa Umoja wa mataifa nchini Libya Martin Kobler alisema kuwa alishangazwa na ripoti za mauaji hayo.

Tupia Comments: